Ofisi ya Rais
Maendeleo ya Vijana
VIJANA WATAKIWA KUCHANGAMKIA FURSA ZA KIUCHUMI, NA...

VIJANA WATAKIWA KUCHANGAMKIA FURSA ZA KIUCHUMI, NANAUKA ASISITIZA UAMINIFU KWENYE MIKOPO.

23 Jul, 2026
VIJANA WATAKIWA KUCHANGAMKIA FURSA ZA KIUCHUMI, NANAUKA ASISITIZA UAMINIFU KWENYE MIKOPO.

Vijana wana nafasi kubwa ya kuleta mageuzi ya kiuchumi, ikiwa watapata taarifa sahihi na kuchukua hatua. Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - Maendeleo ya Vijana, Mhe. Joel Arthur Nanauka wakati alipotembelea Kikundi cha Vijana 'Tunathamini Afya Yako' kilichopo Majimoto, Katika Halmashauri ya Wilaya ya  Mpimbwe.

Kikundi hicho ambacho kwa sasa kina mradi wa duka la dawa za binadamu wenye thamani ya milioni 80, kati ya hizo milioni 50  ni mkopo kiliopewa na halmashauri kupitia mikopo ya asilimia 10.

Mhe. Nanauka amewataka vijana wengine kuiga mfano wa vijana wa kikundi hicho kwa kuwa wabunifu, na wenye uthubutu. Aidha, amesisitiza uaminifu miongoni mwa vijana wanaoungana na kuanzisha vikundi vya ujasiriamali, hasa pale wanapopewa mikopo ya kukuza mitaji yao.

Katibu wa kikundi hicho, Rosemary Venance Soa ametoa shukrani kwa serikali, kwa kuwawezesha vijana kiuchumi kupitia mikopo isiyo na riba na amewasihi vijana wengine kuchangamkia fursa hiyo ili waweze kujiajiri na kujiletea maendeleo.